
Miili ya watoto 2 kati ya 3 iliyofukuliwa Shakahola
Na ALEX KALAMA
MIILI mitatu ilifukuliwa Ijumaa katika Kijiji cha Bethlehemu, msitu wa Shakahola, Kaunti ya Kilifi kufuatia oparesheni ya ufukuaji makaburi inayoendelea.
Inajumuisha mwili wa mama na mwanawe iliyozikwa kwenye kaburi moja, na mtoto mwingine katika kaburi tofauti.
Miili ya watatu hao inafikisha jumla idadi ya 11 waliothibitishwa kufa njaa kutokana na imani potovu ya mchungaji Paul Mackenzie wa Good Information Worldwide.
Ilikuwa imezikwa kwa gunia, jambo ambalo linaibua wasiwasi kuhusu kupatikana kwa miili zaidi.

Imebainika kufuatia oparesheni iliyoanza Ijumaa kufukua makaburi yanayosemekana yamezikwa miili ya wahanga wa imani potovu ya pasta Mackenzie, anayetuhumiwa kuhadaa waumini wake kufunga bila kula ili wafe akiahidi watakutana na Yesu.
Zoezi hilo linaongozwa na mkurugenzi mkuu kitengo maalum kinachoshughulikia masuala ya mauaji, Idara ya Uchunguzi wa Jinai na Uhalifu (DCI), Bw Martin Nyuguto kwa ushirikiano na vitengo mbalimbali vya polisi Malindi, wakiwemo maafisa wa GSU.
Awali, afisa huyo aliambia Taifa Leo kwamba huenda shughuli hiyo ikachukua siku mbili kwa kile alihoji “tumetambua kuwepo kwa makaburi mengi”.
Cha kushangaza, afisi ya chifu i umbali wa kilomita 20 hivi kutoka yalipo makaburi yaliyofukuliwa.
Mchungaji Mackenzie angali anazuiliwa na polisi, uchunguzi ukiendelea kabla kufunguliwa mashtaka.